Feeds:
Posts
Comments

Nilianza kumsikia- Stephen Charles Kanumba- wakati wa joto-joto la – Big Brother  South Afrika 2009- aliposababisha mjadala mkali wa uzungumzaji wa Kiingereza, sanaa, uzalendo,nk.

Marehemu Kanumba akithibisha mapenzi ya kazi yake kwa kushikilia kamera wakati wa kutengeneza filam ndogo ya “Lovely Gamble”  Septemba 2009 na Urban Pulse, Uingereza. Nyuma ni hoteli maarufu la wana Msumbiji- “Nandos.” Picha ihsani ya Urban Pulse, Reading.

Steve Kanumba alikuwa mwigizaji wa kwanza wa Kitanzania kujitokeza nje ya Bongo na mjadala ukawa moja ya matokeo yaliyochomoza kutokana na juhudi zake kisanaa. Wapo waliomcharura kuwa hakuongea Kiingereza sawasawa na waliotetea kwamba uzungumzaji Kiingereza fasaha haukuwa muhimu kuliko kipaji na jasho la mtu. Ila la msingi ni namna alivyojitokeza haraka na kutikisa bendera ya Bongo na waigiza sinema wa Nigeria, Ghana, Afrika Kusini, nk. Continue Reading »

Said Ahmed Mohammed keshatoa zaidi ya vitabu  30 – Riwaya 11 (ikiwepo” Asali Chungu” kigongo chake cha kwanza kilichomwagika uwanjani mwaka 1976), Tamthiliya 7, mikusanyiko minne ya Ushairi na mikusanyiko Saba ya Hadithi fupi ambayo moja wapo ni “Kiti cha Moyoni” alichochangia na Ken Walibora na “Damu Nyeusi” (pia  na Ken Walibora) kikatoka 2007. Mbali na vitabu, Profesa Said ambaye ni mhadhiri wa lugha za Kiafrika chuo kikuu cha Bayreuth, Ujerumani(toka 1997) na keshachapa vitabu vingi vya watoto wa shule za msingi ambavyo lengo lake kufundisha, kutukuza na kujenga lugha na fasihi ya Kiswahili.

Baadhi ya vitabu vyake Profesa Said Ahmed Mohammed – vyote vimechapishwa Kenya.
Continue Reading »

Mradi mkubwa kuunganisha wazungumzaji wa Kiswahili Afrika Mashariki umeanzishwa na magazeti ya Mwananchi na Taifa Leo, Kenya. Ingawa ukiongea na wananchi nyanda mbalimbali Afrika Mashariki na Kati watasema Watanzania “mnaongea Kiswahili kikali”, ” cha moto”, “kizuri, “cha nguvu”, nk – sidhani kama kiutaratibu tunakithamini na kukijenga kama miaka 30 au 40 iliyopita enzi za Mwalimu Nyerere. Kinachozidi kuharibu ni hili suala la Kiswanglish- ambacho hakieleweki kuku, mwiba, gari, kidevu, au jiwe-(ah tuyaaache hayo).
Hivyo hizi ni habari nzuri sana kuendeleza lugha hii kubwa duniani.
Angalia tovuti la -SWAHILI HUB- inayojumuisha waandishi sehemu zote za Afrika Mashariki- kujiunga pamoja kudumisha Kiswahili:

http://www.swahilihub.com


Yes Vijana!!!
Ilikuwa mjini Dodoma Jumatano mchana. Tarehe 19 Oktoba, 2011.
Siku “Yes Vijana” walipotayarisha semina ukumbi wa Hoteli ya Fifty Six katikati ya jiji. Mwenye hoteli huyo alikubali warsha ifanyike pale bila karaha yeyote. Mungu aendelee kumbariki.
Aliyeongoza matayarisho haya alikuwa kijana mwenye moyo na nidhamu na uthabiti.
Remidius Emmanuel wa shirika la “Youth Empowerment and Support” (YES). Shirika hili lisilo la kiserikali lina tovuti yao inayoelezea nguzo na malengo yao. Tazama mwisho wa ukurasa huu.

Mada zilizoongelewa katika warsha hii ni pamoja na Maisha Ughaibuni, Maendeleo ya Kiswahili Tanzania na Afrika Mashariki, Afya na Maendeleo ya binafsi kwa ujumla.

UFUNGUZI…
Tatizo kubwa duniani ni maumivu ya mgongo. Kukaa sana katika viti, kufanya kazi ngumu za sulubu, uvivu au kutembea vibaya. Mazoezi yanaweza kusaidia sana kupunguza adha hii:

KUINAMA HUKU UMELEGEZA MABEGA KWA MUDA WA DAKIKA MOJA KUENDELEA.

MAZOEZI YA YOGA (Toka INDIA) YANA KILA AINA YA MBINU ZA KUUJENGA NA KUUSAIDIA MWILI KUWA KATIKA HALI NZURI. HAPA DADA MMOJA ANAJITOLEA KUWA CHAMBO CHA KUELEKEZA KATIKA SEMINA HIYO.

ZOEZI HILI LINASAIDIA SI TU MGONGO BALI TUMBO NA MIGUU HASA SEHEMU ZA MAPAJA, MAGOTI NA KUJENGA MWILI KUWA SHUPAVU. USIFANYE KABLA YA KUWA TAYARI UMEJIAMSHA LA SIVYO UTAJIUMIZA.

UFAFANUZI WA UHUSIANO WA MAZOEZI NA AFYA YA VIJANA…

MDAU WA KITOTO NIKIJIBU MASWALI MBALIMBALI IKIWEPO HOJA YA VIJANA KUTAKA KUSAFIRI UGHAIBUNI KUSOMA AU KUFANYA KAZI…

Habari za Jumuiya ya maendeleo ya vijana tembelea tovuti yao hapa:

http://yesvijana.org/


MWILI UKIWA SHUPAVU NA AKILI HUFYATA MKIA…


Juisi la Mbuyu ndani ya kitabu cha Miriam Rose Kitunda.

Miriam Rose Kitunda (pichani chini) ni mpenzi mkubwa wa utamaduni wa Kitanzania. Na mapenzi yake hayaishii tu kwa maneno na bla bla.
Kwa miaka mingi amekuwa akiwasaidia Watanzania kughani na kuziremba tovuti na blogu zao bila malipo yoyote. Hii ni kwa sababu kasomea ufundi huu wa kisasa. Halafu amekuwa akitangaza mapishi ya Kitanzania ndani ya tovuti yake www.tasteoftanzania.com Mwaka huu anatazamiwa kutoa kitabu cha mapishi hayo ndani ya kitabu moto moto cha Kiingereza na Kiswahili.

Ukweli hadi sasa tunavyo vitabu viwili tu vilivyoandikwa na Watanzania kuhusu mapishi ya Kibongo. Cha kwanza kilitolewa na Eva Pendaeli Sarakikya (TPH, Dar es Salaam, 1977) na Zarina Jafrejji katoa mapishi ya Zanzibar ( Taste of Zanzibar, Gallery Publications, 2006). Vitabu ni hivi viwili tu vinavyofahamika, vilivyoandikwa na Watanzania. Kwa hiyo ni furaha kubwa kujua kiko kingine jikoni na mekoni.


Mtaalamu wa kodi toka PWC Tanzania, David Tarimo (kulia ) akijadiliana na Mwingereza aliyeishi Afrika Mashariki miaka mingi hata kuongea Kiswahili, John Small (katikati) na mshiriki mwingine. Picha na F Macha

Wawekezaji, wataalam na wafanyabiashara toka kona mbalimbali ulimwenguni wamekaribishwa kwa mkono wa kheri kuendeleza uchumi na maendeleo ya nchi yetu katika kipindi kinachofuatilia miaka 50 ya Uhuru.
Akiongea wakati wa Kongamano la Uwekezaji (“Tanzania Investment Forum 2011″) hoteli bab kubwa ya May Fair jijini London jana Ijumaa, Waziri wa Nishati na Madini, Mheshimiwa William Ngeleja alisema tuko katika kipindi kipya cha maendeleo ya uchumi chenye manufaa kwa wafanyabiashara.

Waziri William Ngeleja akihutubia kongamano. Picha na Baraka Baraka wa Urban Pulse…
Continue Reading »


Tamasha la kimataifa Ubongo Fest kuadhimisha maisha na kazi za mwanamuziki Remmy Ongala litafanyika mjini Dar es Salaam Jumamosi ijayo tarehe kumi, ukumbi wa Leaders, Kinondoni.
Tamasha hilo ambalo linaangukia sherehe za miaka 50 ya Uhuru wa Tanzania litahusisha watumbuizaji toka Uingereza, bara Afrika na wanamuziki maarufu nchini mathalan Twanga Pepeta, Msondo Ngoma, Bendi ya Matimila, Jikhoman, Mrisho Mpoto na Banana Zoro.

Aziza Ongala

Akifafanua habari hizo binti yake marehemu, Aziza Ongala, alisema Ubongo Fest inatukuza kazi za baba yake aliyeimba kuhusu umaskini, ulaji rushwa, maisha, imani, madhara ya UKIMWI na fahari ya Utanzania. Ingawa mwanamuziki huyu aliyebatizwa jina la “Dokta” na wanahabari, alizaliwa Kongo aliigeuza Tanzania kuwa nyumbani na familia yake baada ya kuhamia nchini mwaka 1978 akiimbia bendi ya Mzee Makassy.
“Ubongo Fest” alifafanua Aziza imetokana na neno Dokta Remmy alilotumia kufafanua mtindo wake wa “Bongo Beat” aliouimba na kwamba lengo lake ni kutumia tafrija kuwa jukwaa la wasanii wa kimataifa kuonyesha, kuvumbua na kutukuza vipaji mbalimbali vya watunzi nchini. Aziza na mumewe Mjamaika, Miael McGeachy wanaoishi London wanasema tamasha hili ni kipemgele cha Dk. Remmy Ongala Foundation iliyoundwa karibuni Uingereza kuendeleza kazi za Ramazani Mtoro Ongala. Moja ya matazamio yake ni kujenga shule ya wasanii na watoto yatima Tanzania.
“Lengo letu ni kutoa nafasi kwa wasanii wa Kitanzania kujenga mawasiliano ya kimataifa ili kusaidia ujenzi wa uchumi na utamaduni Tanzania. Ubongo Fest itakuwa mwanga mkubwa wa Kitanzania utakaorodheshwa katika sinema na rekodi. Ni mategemeo kujenga kiu ya soko la wageni kuja kwetu kadri tamasha litakapozidi kuimarika na kufahamika duniani,” wanaeleza.

Miael McGeachy mumewe Aziza Ongala akiwa na Mwenyekiti wa Chama cha Watanzania Uingereza, Said Surur(wa tatu kulia) na mdau wa Kitoto, mjini London kabla ya kuelekea Dar es Salaam kutayarisha shughul ya Ubongo Fest na mkewe na familia ya marehemu Ongala. Picha na Urban Pulse

Soma habari zaidi : http://www.dkremmyongalafoundation.com

Follow

Get every new post delivered to your Inbox.

Join 171 other followers