MAHOJIANO NA DK. IMANI KYARUZI- Mwandishi wa “Mbinu za Ujasiriamali”

- Dk Imani Kyaruzi akiwa na bi. Susan Mzee, katibu wa Chama cha Watanzania Uingereza, katika uzinduzi wa kitabu, Birmingham, Oktoba 2008
Mwaka jana mmoja wa wataalamu na wasomi wetu anayeishi Uingereza Dk. Imani Silver Kyaruzi alitoa kitabu moto moto “Mbinu za Ujasiriamali” kitakachosaidia sana uchumi na akili za Mtanzania hasa yule anayependa kujiendeleza au kufanya biashara. Kitabu hiki kilichotolewa na wachapishaji stadi wa “Mkuki Na Nyota” mjini Dar Es Salaam kina kurasa 50. Nilimhoji…
KITOTO:
Muundo au fani yako ni kuuliza maswali na kupanga vichwa rahisi vya kuelewa kimaneno. (“Je wewe unauza nini?” “ Je unahitaji watu wa kushirikiana nao?”).Twaweza kusema kazi yako ya kufundisha (Mhadhiri, Uingereza) imeathiri muundo wa kuandika kitabu hiki kizuri chenye lugha nyepesi kueleweka?
Dk. Imani Kyaruzi:
Kweli kabisa…niliamua kutumia lugha nyepesi na yenye kueleweka baada ya kugundua kuwa watu wengi (wafanyabiashara) wanashindwa kufuatilia maelezo yaliyomo katika vitabu vya kimataifa vya ujasiriamali. Si Tanzania tu, bali hata hapa Ulaya wafanyabiashara hawana muda wa kusoma madoido ya kisomi yasiyoeleweka! Ila kwa upande mmoja haikuwa rahisi kuandika kitabu hiki kwa lugha kiswahili kwani nina muda mrefu tangu nimeondoka Tanzania na lugha imebadilika sana. Utakuta katika baadhi ya maneno nimejaribu kufikiri katika lugha zote mbili na kutafuta maneno yatakayofaa kuufikisha ujumbe bila kuupotosha.

Dr. Kyaruzi kashikilia mipini miwili ya elimu : kitabu chake na maikrofoni, Birmingham, 2008
KITOTO:
Mwisho kabisa (sura ya
unatoa muhtasari wa maudhui yako.
“…Usisahau kuwa ujasiriamali si kwa ajili ya kutengeneza faida tu! Ningependa kuwasisitiza wajasiriamali wengine waibuke wenye nia ya kugusa masikini, walemavu na wale wasiojiweza.” Unasisitiza biashara yenye wajibu sambamba na biashara ya faida. Je unakubaliana na mawazo “mapya”nchi za Magharibi karibuni kuwa na ubepari na biashara yenye hisia (compassionate capitalism au responsible capitalism) baada ya matatizo ya uchumi kutokana na mabenki kuanguka (2008-2009)?
Dk. Imani Kyaruzi:
Ilinibidi nisisitize suala la umuhimu wa ujasiriamali-jamii (social entrepreneurship) baada ya kugundua kuwa kuna dhana potofu ya maana sahihi ya ujasiriamali. Watu wengi wanafikiria sana faida badala ya kuboresha maisha ya watu na mazingira yanayowazunguka. Si lazima kwa mfanyabiashara kutoa fungu la kumi, lakini mawazo yangu yanalenga hasa kwa Wafanyabiashara wanaotajirika sana na kusahau kuwa sehemu kubwa ya mapato yao yanatoka kwenye jamii.
Kutikisika kwa uchumi 2008/9 kunaashiria kwamba ubepari-mkomavu hauna nafasi katika kujenga uchumi na maisha bora (hasa kwa kina kabwela). Inasikitisha sana kuona kuwa Afrika na labda niongelee Tanzania yetu tunashindwa kuwa na ubepari wetu (African Capitalism) – ule usiolenga kuwajenga wachache na kuumiza walio wengi. Tutangaze rasmi kuwa ujamaa umezikwa, lakini mbadala usiwe ubepari wa magharibi. Kwanza, ubepari umejengwa na misingi au dhana potofu ya kutengeneza fedha na utajiri wa harakaharaka wenye vyanzo tata (mfano “EPA-ism”). Pili, ubepari-mkomavu umepoteza uhalisia – wachache walishachukua nafasi za peponi hivyo ukiona leo Wazungu wanalima bustani za mboga badala ya kwenda sokoni hii inaashiria kuwa tunaanza kurudi ardhini na ni jambo zuri kwa dunia ya tatu kwani mzani unalegea pande zote. Hii ndio maana yangu ya uhalisia – ya kwamba si vibaya tukitegemea sekta ya huduma, tukashinda tunalonga kwenye Tigo na Voda na matumizi ya tovuti lakini tukakumbuka kuwa kama “ukitaka mali utayapata shambani” – si vibaya kutumia mikono. Tufanye kazi kwa bidii na hakuna mbadala wa kazi na ubongo.
KITOTO:
Je umeonaje matokeo ya mkutano wa G20 ambayo yameonyesha nia hiyo kupitia Rais Barack Obama wa Marekani?
Dk. Imani Kyaruzi:
Nina hakika G20 itakuwa na matokeo mazuri pindi maazimio yaliyofikiwa yatakapowekwa katika vitendo. Mikutano hii mikubwa huja na ahadi nyingi na tabasamu nene na picha za watu mashuhuri waliovaaa suti kali hivyo sitaliongelea sana suala hili hadi pale vitendo vitakapoanza kutendeka.
Suala moja walilolisahau kwenye G20 ni kuwahimiza watu wa Afrika kuwa wakaze uzi, waache uvivu na wapunguze utegemezi kwani jungu la wafadhili ipo siku litatakauka na watalala njaa kwa kuendekeza tabia ya kuombaomba. Siku ikifika kila mtu atajali watu wake kwanza na sio wananchi wa Mwanalugali! Tusiweke misaada ya wafadhili kama sehemu mojawapo ya miundo ya kujenga uchumi bora – hii dhana imepitwa na wakati.

Dk Kyaruzi akimkabidhi Balozi Mwanaidi Maajar nakala ...
KITOTO:
Turudi katika uandishi Tanzania. Mkuki na Nyota ni wachapishaji pekee wanaowakilishwa kidogo nje, wenye tovuti na wanaojitahidi. Je kitabu kinauzwa vizuri? Ulichapisha nakala ngapi? Je, wasomaji wengi wako nje au ndani? Unayo njia ya kuyajua hayo?Unaridhishwaje na hali ya uandishi na usomaji wa vitabu nchini.
Dk. Imani Kyaruzi:
Mkuki na Nyota wanao mpango wa kukiendeleza na kukisambaza kitabu hiki nchini kote. Kazi hii imeanza tayari na ninategemea mawasiliano hivi karibuni. Nakala zilizochapishwa ziko katika maelfu na ninaweza tu kuongelea wanunuzi wa bara la Ulaya. Wakati wa unzinduzi nilifanikiwa kusaini nakala nyingi sana na kitabu kilipokelewa vizuri na umati wa Watanzania waishio Uingereza. Baadhi ya nakala zilienda Ujerumani kwa wasomaji wa huko na marejesho yanaridhisha.
Nia ni kuwafikia wasomaji wa ndani na kazi hii itaanza baada ya majuma mawili. Ningependa kutoa mafunzo nyumbani wakati wa kukitangaza kitabu hiki.
Kuhusu uandishi na usomaji, inasikitisha sana kwani tumezoea kuona vitabu vya kina Michael Porter na kina Mr Smith na ninafikiri Watanzania tukianza kuandika italeta changamoto kwa waandishi walioko nyumbani ambao naamini wako wengi, tu. Kwa upande wa usomaji sina uhakika na hilo, ila tu ningependa kusisitiza kuwa vitabu vya mitaala hadi Chuo Kikuu viwakilishwe na vitabu vilivyoandikwa na wazalendo na vyenye kulenga katika hali halisi ya nchi. Hii ni muhimu kwani vitabu vyenye maudhui ya Kiulaya vinawatayarisha vijana wetu kutumikia nchi gani?
KITOTO:
Nini makusudi ya kuandika kitabu kuacha yale uliyoelezea mwanzoni (Utangulizi). Je, nini kilichokupa moyo au nia ya kuandika kitabu. Labda uliona hatusomi? Labda uliona wafanyabiashara Ulaya (kama bwana Richard Branson uliyemtaja) wanaandika vitabu?
Dk. Imani Kyaruzi:
Wakati wa ziara ya utafiti barani Afrika (Tanzania, Uganda, Ghana, Swaziland na Botswana) niligundua baadhi ya vitu vilivyokuwa vikkikwamisha biashara za wazalendo. Watu walikuwa wema sana na walichangia mawazo nami nilihaidi kutumia mapungufu yao, si kwa kuwaonyesha kuwa hawawezi bali kuwarudishia kitu fulani ambacho wanaweza kukitumia kuendeleza biashara zao. Je, ujumbe ningeufikishaje wakati walio wengi hawaongei lugha za kigeni? Nilionelea ni vyema kuanzia nyumbani, hivyo nikajikuta ninaandika kwa Kiswahili. Nia haikuwa kutengeneza faida bali kurudisha kitu kidogo katika jamii iliyonilea kwa mapenzi makubwa. Pia kuna wale watu wenye nia njema ya kujenga uchumi wetu lakini hawakubahatika kwenda vyuoni na wana nia ya kujiendeleza – hawa wanahitaji msaada wetu mkubwa kwani kama wote tungefanikiwa kwenda vyuoni basi baadhi ya biashara zisingekuwepo! Mama Ntilie aliyenipikia nikiwa Tambaza na Mzee Sefu wa Chips nao pia wasingenipatia lishe bora iliyonisukuma hadi leo naweza kuitwa Bwana Daktari. Lakini jambo muhimu hapa ni kwamba si lazima uende chuo kikuu kujifunza namna ya kutathmini faida katika biashara, unaweza kusoma kitabu hiki na kufuata mifano…
Dr. Imani Kyaruzi ni Profesa Msaidizi katika Chuo Kikuu cha London Graduate School of Management…
KITOTO:
Sura ya Tatu muhimu sana; maana unaeleza “namna ya kupanga biashara.” Mantiki yako kwa maoni yangu mpitiaji ni kudokeza juu ya uholela na kutokuwa na nidhamu katika masuala yetu ya kikazi Bongo. Unafikiriaje kuhusu wafanyabiashara wetu. Je wana nidhamu, bidii na kujituma? Mbona Wakenya, Waganda na Wahindi wanatawala sana biashara zetu Tanzania?
Dk. Imani Kyaruzi:
Hii imenifurahisha sana! Kuna biashara za aina nyingi Bongo lakini zinazotawala ni zile za kina bwana Kauzeni – hajui tofauti ya rafiki na mteja, msambazaji na mzalishaji n.k Wote hawa huwaweka kundi moja na hata mtaji hajui alianzia wapi na kuishia wapi. Mifumo mingi ni kama ya genge – nyaya zikija unanunua tenga – zote mbivu, mbichi na zilizooza ; siku zikiharibika mtu anasema ni kudra ya Mungu, zikiuzwa zote anasema ridhiki imeingia. Watanzania wanajituma sana, tatizo ni nidhamu katika kazi na huduma kwa wateja. Waganda, Wakenya na Wahindi wanaweza sana kutawala biashara zetu kwani utamaduni wao unatofautisha biashara na sindimba. Wakiwa katika biashara uhusiano wao hubadilika na hufuata kanuni za biashara na wakati wa sindimba kanuni zinazotumika ni zile za midundo. Lakini tumeanza kubadilika – tunaweza kujifunza kutoka kwa hawa wenzetu; ila tusijifunze kila kitu kwani tabia zingine za wageni si za kuiga.
KITOTO:
Je unaamini ubepari utaleta maendeleo Tanzania? Yaani ukilinganisha enzi za Ujamaa (1967-1986) na Mwalimu Nyerere?
Dk. Imani Kyaruzi:
Duh! Tanzania sio nchi ya Kijamaa na wala sio nchi ya Kibepari bali iko tu katika hatua za kusahau nasaha za ujamaa na kuuelekea ubeparini – tumeacha tu kuvaa kaunda suti lo! Kutokuwa na msimamo kamili ndo’ kunaleta utata juu ya faida na hasara za mifumo hii katika kuleta maendeleo. Kuna vitu viwili hapa – siasa zinajenga uchumi au uchumi unajenga siasa. Bwana mwandishi enzi za Nyerere siasa za ujamaa zililenga katika kujenga uchumi ulio bora na wenye uwiano. Sasa baada ya kifo cha ujamaa hadi leo hii uchumi ndio unaamua siasa gani ufuate! Sasa tukirudi katika swali lako jibu ni hapana na ndio! Ubepari utaweza kuleta maendeleo kwa watu wachache tu wanaojua kucheza katika anga za ubepari, walio wengi hawajui na hawatajua nini kinaendelea na wanaweza kuuzwa kwa bei ya jumla. Ubepari nia yake ni kulimbikiza mali na si rahisi kujenga uwiano – hapa ni rahisi kujenga jamii mbili za wazalishaji na walaji na mara nyingi masikini ndio wanakuwa wazalishaji. Kwa upande wa pili, ubepari unaweza kuleta maendeleo kwa kuendeleza ushindani. Kama nilivyoeleza katika kitabu, ushindani ni wa muhimu sana katika kujenga jamii yenye ari ya kujituma na kuzalisha bidhaa na huduma bora. Tatizo labda la huu ushindani ni kuwa mara nyingi unakuta washindanaji wana nguvu zisizowiana – kwa mfano Steers na Mama Hassan wa Sinza wakiamua kutengeneza vitumbua Mama Hassan atashindwa kwani hajaendelezwa au kuwezeshwa japo kufikia nusu ya kiwango cha mshindani wake. Maana yangu ni kwamba kabla hujaruhusu ushindani nyumbani kwako lazima uhakikishe wapiganaji wako umewalisha vizuri la sivyo nyumba yako inaweza kutawaliwa na wageni.
Sasa nini kifanyike! Kwa mtazamo wangu ubepari si mbadala halisi wa ujamaa. Baada ya mfumo wa ujamaa kufumuka tulitakiwa kusuka mfumo wetu wa ubepari ambao hauna matobo mengi kama tulionao sasa. Huu mfumo wetu wa sasa wa Pseudo-capitalism au wengine wanaita a transition to a market-led economy misingi yake ni ile ya kula kuku, mayai, manyoya na hata mbolea kistaarabu huku wananchi wakizidi kuumia. Maendeleo ya ubepari utayaona Oysterbay na Masaki lakini huko Mwanalugali sahau kabisa – maendeleo yatakuwa ni barabara za kupitisha mchanga wa kujenga nyumba za mapumziko ya wikiendi. Tutataendelea kupita huku watoto wadogo wenye kamasi vifua wazi wakiendelea kupungia magari yetu makubwa kama nyumba. Hatutasikia kelele zao kwani vioo vitakuwa vimefungwa ili hewa iliyochujwa isichanganyike…
WASILIANA NA MWANDISHI KUPATA NAKALA AU HABARI ZAIDI :
Simu : +44 -7977807295
Barua pepe: boraimani@yahoo.com