Feeds:
Posts
Comments

Jamii zetu zinazoendelea zinahitaji sana Elimu.  Elimu itakayotusaidia kupambana na maadui kama : kutojua kupanga muda (Time Management) tatizo linalotufanya tuchelewe, tusiwe na mpangilio wa maisha ; halafu, kutoyajali mazingira yetu (vyoo vichafu na kutupa taka ovyo).Uchafu wa mazingira DarWataalamu wameshatuonya kuwa makaratasi ya plastiki tunayoyaacha kiholela kila mahali (yenye madawa hatari) yanaharibu rutuba na uhai ; yatakaa ardhini miaka 500 !!!

Bougainvillea -Silversands

Si mbali  na palipotupwa plastiki hizi pana hoteli hii marufu na nzuri ya Silversands ambapo watalii na wenye uwezo wanakaribishwa kwa maua  mazuri yenye asili ya Kimarekani yaitwayo Bougainvillea.  Ikiwa tunaweza kuyapamba mazingira ki-azizi,  hatushindwi kuyaacha safi…

Madafu

Nilishangazwa nilipoelezwa na muuza madafu mmoja Dar kuwa kinywaji (chakula) hicho muhimu siku hizi hakipatikani kirahisi. “Minazi inakatwa ovyo…” akalalama. 

Minazi ya Dole

Nilipokuwa kitongoji hiki cha Dole, Unguja, nikawa nawaza lile balaa la minazi kukatwa bandari  ya Dari Salama. Minazi imesimama dede mithili ya twiga au mbuni malishoni.  Je, itadumu? 

Matunda ya Afrika  Sehemu nyingi Zanzibar bado vyakula asilia vinathaminiwa. Cheki  matunda, mboga na makulaji : mjini na vijijini. Ama kweli inatia moyo…maana chakula ni utamaduni wa nchi; kama huna au unaiga (huthamini chako) huna jicho…

Chakula cha Zanzibar

Huku unakula huku unafikiria namna ambavyo bado wananchi wengi tunatupa chupa za maji ovyo nje; tunavyofungia bado vyakula vyetu kwa magazeti badala ya mifuko isiyokuwa na sumu na madawa… 

Chupa ya maji- uchafu

Kinamasi hiki kimejaza si tu plastiki  na dawa zenye sumu bali pia wadudu kama mbu. Kila anayeweza (kutumia mtandao na kompyuta ni uwezo na nafasi) kuelemisha watu wetu ajitahidi na kujaribu…maana hizi blogu hazisomwi na wengi.

Silversands-2

Hapa natia tizi katika moja ya bichi za Dar…ukweli si rahisi siku hizi kupata ufukwe msafi mjini hapa. Na hata zile safi baada ya kuogelea unahisi macho yakikuwasha washa. Watalaam wameonya kuhusu kutupa taka ovyo baharini, kunya (na kukojoa) ovyo ufukweni, kuchafua michanga kwa vyupa vya vinywaji tunapostarehe kando ya bahari mama ya Hindi.

Jani la Mnazi

Pwani ya Dar

DSCI0168

Zoezi maalum la kusaidia mabega kutokana na kazi mbalimbali zinazoathiri migongo, shingo na kichwa. Kuning’iniza bega moja ukizungusha mkono pande zote, huku mkono mwingine umeshika kiti au meza. 

Semina zilitayarishwa na jarida la LUCKY linaloendeshwa kwa ushirikiano wa wananchi wanaojitolea mhanga kuelemisha na kuendeleza jamii ya Tanzania.  Waliosimamia kazi hii ni Innocent Swai na mhariri wake Anna Rugaba. Zilifanyika Ukumbi wa British Council, Shule ya Sekondari Mwandege, Pwani; Nyumba ya Sanaa na Soma Cafe, Mikocheni.

 Nilialikwa kuendesha mada nne muhimu:

1-Maisha ya Ughaibuni : utamaduni, elimu, kazi, uzoefu nk.

2-Afya, Chakula na Mazoezi ya mwili na viungo kwa jumla

3-Uandishi, fasihi na umuhimu wa kusoma na vitabu

4-Muziki : utunzi, uimbaji, upangaji na sanaa

5-Kitabu changu “Mpe Maneno Yake”

WKshops Dar -6

Mazoezi ya viungo, Ukumbi wa Vijana wa Tayoa (Tanzania Youth Alliance) Nyumba ya Sanaa.

WKshops Dar -8

DSCI0196

DSCI0171

Zoezi la kunyoosha mwili linalotokana na mfumo wa Yoga unaolinganisha kiwiliwili na mti (Tree Pose). Manufaa yake ni kukupa mwili usiojipinda ili kupunguza maumivu ya mgongo, kiuno na mabega. Pia husaidia akili , moyo na ari.

Baada ya semina Shule ya MwandegeWanafunzi  waliojaa hamasa  Shule ya Sekondari Mwandege, baada ya semina waliyovumilia saa tatu nzima. Mseto wa muziki, fasihi, rapu, mazoezi nk. (Picha na H. Macha)

Washiriki Bri Council mada ya Ughaibuni

Washiriki mada ya Maisha Ughaibuni, ukumbi wa British Council, wakiandika hoja. Maswali na majadiliano yalikuwa mengi. (Picha na Innocent Swai)

Mazoezi ya Kichwa- Mwandege

Mazoezi ya shingo Shule ya sekondari Mwandege yenye vidato vinne (Picha na H. Macha)

Anna Rugaba- Br CouncilAnna Rugaba wa  Lucky Magazine -Ideas for Living - lililotayarisha warsha hizi akisaidia washiriki kutoa maoni na mrejesho nyuma. (Picha na Innocent Swai)

Asha Mtwangi na mwenzake- Soma Cafe 

Washiriki Soma Cafe : Asha Mtwangi  wa Futures Group (www. futuresgroup.com) linalohamasisha vijana, afya na tamthiliya akiwa na Shanande Mushi…

Anna Rugaba akijaribu zoezi la paka- Yoga

Mshiriki na mtayarishaji Anna Rugaba wa Lucky akijaribu zoezi la kujinyoosha la Yoga mtindo wa Paka (Cat pose) ambalo husaidia viungo vingi ukiwemo mgongo, tumbo, miguu, mikono, mabega, mapigo ya moyo, kizazi na akili.

Asha Mtwangi (kushoto) na mwandishi chipukizi, Soma CafeWaliohudhuria semina Soma Cafe ambapo suala la kusoma vitabu linafanyiwa kazi na kampuni ya E & D Limited pale Mikocheni. Kushoto ni Asha Mtwangi na kulia ni mwandishi chipukizi,  Shanande Mushi.

Swai na viongozi wa Tayoa 

Innocent Swai wa Lucky Magazine- Ideas for Living- akiwa na viongozi wahamasishaji wa Tayoa (Tanzania Youth Alliance) wanaosaidia magonjwa ya zinaa katika Nyumba ya Sanaa.   Hawa walitukaribisha kwa mikono yote wakatupa ukumbi bure siku tatu. Katikati ni Meneja Mawasiliano, Benedicto Luvanda, mchapa kazi aliyehakikisha shughul hii inafanikiwa toka mwanzo hadi mwisho.

Prof Mulokozi, Soma Cafe

Kati ya wanafasihi wenye uzoefu mkubwa nchini ni Profesa Muyagbuso Mulokozi aliyehudhuria semina ya Soma Cafe. Baada ya kuwaeleza vijana kuwa mtaalamu huyu alikuwa kati ya wahamasishaji wangu wakubwa nikiwa naanza kuandika miaka ya Sabini  baadhi walikaa wakimsikiliza. Hapa Prof Mulokozi anatoa store kuhusu gwiji wa fasihi ya Kiswahili Shaaban Robert.

Ibrahim Boss -Kit drummer

Mwanamuziki mkongwe, Ibrahim Boss, aliyekuwa zamani mpiga ngoma (kit drums) bendi ya Revolutions (Kilimanjaro Hotel) miaka ya 80 alikuwepo Soma Cafe. Alisaidia pia kuchangamsha ngoma wakati  nikitumbuiza kwa gitaa na nyimbo.

DSCI0147Mwalimu Mkuu wa Shule ya Mwandege Boys, Bw. Enock Walter na baadhi ya wanafunzi viongozi. Shule hii isiyotumia kengele ni kati ya shule za kipekee nchini zinazotoa elimu inayowatayarisha wanafunzi kuwa makini zaidi kinidhamu, kitabia na kiakili.

Wkshops -11

Nyumba ya Sanaa…

Muziki Mwandege Sec School

Muziki wa gitaa, mashairi na fasihi

Majadiliano Fasihi

Majadiliano kuhusu fasihi, maisha ughaibuni, afya; maswali na majibu:  Nyumba ya Sanaa…

Karibuni nimeingia tena Bongo baada ya miaka miwili. Ama kweli kwa tunaoishi ughaibuni kurudi nyumbani ni kama kwenda hospitali. Kabla ya tiba lakini, shurti  kuujua ugonjwa.

Swai, FM, na Michuzi- Nyumba ya Sanaa

Tiba ya kwanza utani, masihara na vicheko.  Hapa tuko Nyumba ya Sanaa (iliyofunguliwa na Mwalimu Nyerere mwaka 1983); leo imegeuzwa Jumba La Kila Kitu : baa, kamari, michezo, hoteli, mahali pa watalii kununua vito vya Tanzania, makutano kwa walioko mjini; kuchaji simu za mkononi, kutazama mpira mathalan ligi za Ulaya; sehemu ya kufanyia mazoezi na maonyesho.

Niko na Al Watan,  baada ya kuchapa nyama choma kwa ndizi choma na vinywaji.  Kwanza kabisa ni Innocent Swai mhamasishaji, mjasiriamali na mwendeshaji wa jarida jipya la “Lucky”;  kushoto kwangu ni Issa Michuzi  mpiga picha na mwanablogu maarufu siku hizi. (Picha na Blandina Kilama)

….Tiba ya kwanza ukirudi nyumbani ni vicheko. Unafurahia usiowaona muda mrefu.  Swali la kwanza: je, utacheka  muda gani?

Msukuma mkokoteni Magomeni, dar

Barabara itokayo Magomeni kwenda Ilala; hapa kuna mfano mzuri wa jiji la Dar leo. Magari makubwa makubwa aina zote : Pajero, Prado, nk. Barabara zilizopanuliwa; mioshi ya magari na vumbi; hapo hapo huyu bwana mgongo wazi akivuta mkokoteni  (kwa baiskeli) akitafuta ajira. Mbio za mapanya zimeingia Bongo kiasi wahisi kila kitu mwendo mkali… 

(picha ya mdau wa Kitoto)

Karibu  ndani; karibu chakula….sikiliza  moja ya nyimbo zangu penzi unaoongelea  namna mbalimbali za Uhuru; … na jinsi Uhuru ulivyo muhimu kuliko kitu kingine chochote duniani.

Niliutunga mwaka 1980 wakati  bado naishi “geto” moja pale Mwananyamala Kisiwani, Dar es Salaam.  Usiku nilioupika sikulala kutokana na kilio cha mwanamke aliyekuwa akikandikwa makonde,  mateke, matusi na mumewe aliyemkuta kaomba Sabuni toka kwa jirani sababu ya hali ngumu ya uchumi. Ongeza pia kwamba kipindi (enzi hizo) hakukuwa na uhuru wa kusema au kujieleza kama leo….

Wanaopiga nami kushoto piano -Kaz Kasozi ( Uganda) ;  besi- mdau mwenzangu wa Kitoto, Andre Mathurin (visiwa vya St Lucia); tumba (congas) -Trevor Antonio mwenye asilia ya Kiafrika na Kijamaika.

Aliyesimamia kazi hii ni Kaz Kasozi mwenyewe akishirikiana na  Krawl (kamera): marafiki na ndugu katika muziki, maudhui na sanaa….

Kasozi ambaye ana vipaji vingi alikuwa pia fundi mitambo wa CD yangu ya mwaka 2000 : “Constipation…”

stairs“ELIMU HAINA MWISHO…”

Methali ya Kiswahili

 Nchi yetu ina utata.

Mheshimiwa Rais kachorwa vibaya mitandaoni; miezi kadhaa iliyopita akazomewa ilhali kachaguliwa kwa asilimia 80 ya kura; Rais wa zamani, bwana Mwinyi akapigwa kofi hadharani; ajali za mabasi zimezidi,uvutaji bangi (hasa miongoni mwa vijana) umefikia asilimia 90 sehemu fulani fulani; viongozi mafisadi mahakamani; utovu wa nidhamu unaiandama nchi yetu ya Tanzania.

Tumeshasikia Muziki wa Kizazi Kipya ; tunahitaji pia Mawazo ya Kizazi Kipya: Wachapa kazi wa Kizazi Kipya; wananchi wenye nidhamu na mwenendo utakaodumisha amani na maendeleo ya Tanzania.

 

innocent-swai-by-mugeta-mwendwa

…Tulitazame jarida jipya la Lucky, lililoanzishwa karibuni mjini Dar es Salaam.

Mhamasishaji Innocent Flugence Swai,  (pichani) mwalimu wa kompyuta, mjasiriamali, msomi anayeamka saa kumi na moja kila siku alikuwa na  haya machache…

 

FM:

Je  magazeti yanawezaje kusaidia changamoto na maendeleo ya Mtanzania? 

 SWAI:

Ninaamini kwamba majarida kama Lucky! Yana uwezo wa kuleta mwamko. Ni rahisi sana kulaumu, kulaumiwa na kulaumiana. Lakini tunaweza kujenga mawazo mbadala

 FM:

Jarida lenu  lina makala za mseto. Ipo  inayowaasa wanawake kutovaa sidiria zisizofaa, pana mahojiano na msanii Mrisho Mpoto halafu makala ya elimu yenye picha zenye watoto wakiwa darasani. Mmegusia pia tatizo la Ma Albino. Makusudio ni nini hasa?

 SWAI:

Tanzania ina matatizo mengi mno! Ni vigumu kwa ulimwengu huu wa sayansi na teknolojia kugusa tatizo moja,  ndiyo maana tunaweza kuwa na malengo tofauti tofauti huku tukigusa matatizo kadha wa kadha ili kila mtu na hitaji lake tofauti apokee kitu toka kwetu.

 

 

 

green-grass

 FM:

Lucky pia  lina lugha mbili, yaani Kiswahili na Kiingereza. Mkondo huu umeanza sana kukua katika nyendo za majarida ya kisasa Bongo. Je ni muhimu?

 SWAI:

Ni muhimu, ni muhimu sana, manake ni jamii ambayo bado hatuna nguvu ya kumudu hizi mbili tu. Pia tunawalenga watu toka nyanda zote za jamii; hivyo ni muhimu kuhakikisha kila mmoja, mdogo kwa mkubwa pasipo kujali elimu, rangi, kipato, au itikadi anahamasishwa na jarida letu.

 

JITAFUTIE NAKALA YAKO YA LUCKY; UTAJIFUNZA LUGHA; UTAPATA HOJA MPYA; IKIWEZEKANA UNAWEZA HATA KUWAANDIKIA.

 “UJASIRIAMALI SI LAZIMA IWE KAZI YA MTU MMOJA AU WAWILI, BALI KUNA WAKATI AMBAO KUNDI LA WAJISIRIAMALI HUJIUNGA PAMOJA NA KUANZISHA KAMPUNI MOJA YENYE NIA MOJA.”

-Dk Imani Kyaruzi, Profesa Msaidizi Chuo Kikuu cha London Graduate School of Management.

 “KIPIMO CHA THAMANI YA MWANADAMU NI KIASI CHA FURAHA ALIYONAYO. AKIENDELEA FURAHA YAKE PIA HUWA KUBWA.”

-Bruce Lee, Mwigizaji sinema, Mpiganaji Gung Fu, Mwanafasalfa, 1963.

 

 

 

 

 

jj-at-work2JJ Otieno akiwa kazini Brixton, London, 2007 (picha na F. Macha)

 

Kwa miaka lukuki Waafrika tumeonyeshwa ovyo ovyo sana katika runinga na vyombo vya habari duniani. Mtazamo ulioenea ni kuwa tunakufa njaa, tunapigana wenyewe kwa wenyewe na taswira iliyozoeleka ni ya watoto wenye mainzi machoni, wanawake wenye matiti yaliyoanguka wanaobeba magunia, kina baba wanaotembea miguu mitupu, majeshi na viongozi wenye vitambi wasiojali maslahi ya wananchi…Aghalabu… ndiyo sababu ya kuanzishwa Africans in London TV Uingereza, kujaribu kuachana na maono haya muflis…Bahati mbaya kama hutumii mtandao au iwapo kompyuta yako haina ”Media Player” si rahisi kuiona runinga hii. Kwa sasa bado ni runinga ya mtandaoni. Lakini haitakuwa hivyo muda mrefu…Africans in London TV (AILTV)  imeanzishwa na Mkenya Joseph Adamson akishirikiana na baadhi ya wanamuziki Waafrika tunaoishi mjini hapa nikiwemo mwandishi wa blogu ya Kitoto.

AiLTV ilivyoanza ilikuwa hivi mwaka 2007…

 

Bwana JJ ( kama anavyojulikana) mwanamuziki, fundi mitambo na  mwendeshaji mkuu anafafanua katika kurasa nne nzima za mahojiano na jarida la televisheni TV-BAY karibuni  kuwa lengo letu kuu ni kuitumia teknolojia vyema. Kaeleza pia kwenye barua iliyotolewa na makao makuu ya runinga za mtandaoni mjini Brighton Uingereza yaani IPTV Chanell :

“…Vipindi vyote vya AILTV vitatengenezwa na watu wenye asili ya Kiafrika, kuhusu watu wenye asili ya Kiafrika, au kuonyesha maslahi na utamaduni  wa watu wenye asili ya Kiafrika.”

Kutokana na juhudi zetu moja ya kampuni bab kubwa zinazotangaza urembo nchini Uingereza ”Brand Design Agency” (BDA) imeahidi kuisaidia AilTV inayofanya kazi bila pesa na kwa kujitolea bado, kusimama dede…

 

 Hebu angalia baadhi ya vipindi hapa; uwe na subira kama picha zitakwama au pole pole kutegemea na kompyuta unayotumia:

http://ailtv.gdbtv.com/player.php?rand=853&h=a431593a04b99572ab390b80e596b75e&TID=05defa40f8aa04e24ce986554fca7684

 Je unataka kutengeneza vipindi vya runinga? Je unayo sinema? Jaribu kufanikisha ndoto zako kwa kuwasiliana nasi. Tutumie video fupi (demo) isiyozidi dakika tano kuonyesha mfano. Tuko pamoja.

Tuwasiliane:

josephadamson62@yahoo.com

Simu: +44-7595 040-952

+44-7986375-992

Au

kitoto2004@yahoo.co.uk

+44-7961 833040

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

MAHOJIANO NA DK. IMANI KYARUZI- Mwandishi wa “Mbinu za Ujasiriamali”

Dk Imani Kyaruzi akiwa na bi. Susan Mzee, katibu wa Chama cha Watanzania katika uzinduzi wa kitabu chake, Birmingham, Oktoba 2008.
Dk Imani Kyaruzi akiwa na bi. Susan Mzee, katibu wa Chama cha Watanzania Uingereza, katika uzinduzi wa kitabu, Birmingham, Oktoba 2008

Mwaka jana mmoja wa wataalamu na wasomi wetu anayeishi Uingereza Dk. Imani Silver Kyaruzi alitoa kitabu moto moto “Mbinu za Ujasiriamali” kitakachosaidia sana uchumi na akili za Mtanzania hasa yule anayependa kujiendeleza au kufanya biashara. Kitabu hiki kilichotolewa na wachapishaji stadi wa “Mkuki Na Nyota” mjini Dar Es Salaam kina kurasa 50. Nilimhoji…

KITOTO:

Muundo au fani yako ni kuuliza maswali na kupanga vichwa rahisi vya kuelewa kimaneno. (“Je wewe unauza nini?” “ Je unahitaji watu wa kushirikiana nao?”).Twaweza kusema kazi yako ya kufundisha (Mhadhiri, Uingereza) imeathiri muundo wa kuandika kitabu hiki kizuri chenye lugha nyepesi kueleweka?

Dk. Imani Kyaruzi:

Kweli kabisa…niliamua kutumia lugha nyepesi na yenye kueleweka baada ya kugundua kuwa watu wengi (wafanyabiashara) wanashindwa kufuatilia maelezo yaliyomo katika vitabu vya kimataifa vya ujasiriamali. Si Tanzania tu, bali hata hapa Ulaya wafanyabiashara hawana muda wa kusoma madoido ya kisomi yasiyoeleweka! Ila kwa upande mmoja haikuwa rahisi kuandika kitabu hiki kwa lugha kiswahili kwani nina muda mrefu tangu nimeondoka Tanzania na lugha imebadilika sana. Utakuta katika baadhi ya maneno nimejaribu kufikiri katika lugha zote mbili na kutafuta maneno yatakayofaa kuufikisha ujumbe bila kuupotosha.

Dr. Kyaruzi kashikilia mipini miwili ya elimu : kitabu chake na maikrofoni, Birmingham, 2008

Dr. Kyaruzi kashikilia mipini miwili ya elimu : kitabu chake na maikrofoni, Birmingham, 2008

KITOTO:

Mwisho kabisa (sura ya 8) unatoa muhtasari wa maudhui yako.

…Usisahau kuwa ujasiriamali si kwa ajili ya kutengeneza faida tu! Ningependa kuwasisitiza wajasiriamali wengine waibuke wenye nia ya kugusa masikini, walemavu na wale wasiojiweza.” Unasisitiza biashara yenye wajibu sambamba na biashara ya faida. Je unakubaliana na mawazo “mapya”nchi za Magharibi karibuni kuwa na ubepari na biashara yenye hisia (compassionate capitalism au responsible capitalism) baada ya matatizo ya uchumi kutokana na mabenki kuanguka (2008-2009)?

Dk. Imani Kyaruzi:

Ilinibidi nisisitize suala la umuhimu wa ujasiriamali-jamii (social entrepreneurship) baada ya kugundua kuwa kuna dhana potofu ya maana sahihi ya ujasiriamali. Watu wengi wanafikiria sana faida badala ya kuboresha maisha ya watu na mazingira yanayowazunguka. Si lazima kwa mfanyabiashara kutoa fungu la kumi, lakini mawazo yangu yanalenga hasa kwa Wafanyabiashara wanaotajirika sana na kusahau kuwa sehemu kubwa ya mapato yao yanatoka kwenye jamii.

Kutikisika kwa uchumi 2008/9 kunaashiria kwamba ubepari-mkomavu hauna nafasi katika kujenga uchumi na maisha bora (hasa kwa kina kabwela). Inasikitisha sana kuona kuwa Afrika na labda niongelee Tanzania yetu tunashindwa kuwa na ubepari wetu (African Capitalism) – ule usiolenga kuwajenga wachache na kuumiza walio wengi. Tutangaze rasmi kuwa ujamaa umezikwa, lakini mbadala usiwe ubepari wa magharibi. Kwanza, ubepari umejengwa na misingi au dhana potofu ya kutengeneza fedha na utajiri wa harakaharaka wenye vyanzo tata (mfano “EPA-ism”). Pili, ubepari-mkomavu umepoteza uhalisia – wachache walishachukua nafasi za peponi hivyo ukiona leo Wazungu wanalima bustani za mboga badala ya kwenda sokoni hii inaashiria kuwa tunaanza kurudi ardhini na ni jambo zuri kwa dunia ya tatu kwani mzani unalegea pande zote. Hii ndio maana yangu ya uhalisia – ya kwamba si vibaya tukitegemea sekta ya huduma, tukashinda tunalonga kwenye Tigo na Voda na matumizi ya tovuti lakini tukakumbuka kuwa kama “ukitaka mali utayapata shambani” – si vibaya kutumia mikono. Tufanye kazi kwa bidii na hakuna mbadala wa kazi na ubongo.

KITOTO:

Je umeonaje matokeo ya mkutano wa G20 ambayo yameonyesha nia hiyo kupitia Rais Barack Obama wa Marekani?

Dk. Imani Kyaruzi:

Nina hakika G20 itakuwa na matokeo mazuri pindi maazimio yaliyofikiwa yatakapowekwa katika vitendo. Mikutano hii mikubwa huja na ahadi nyingi na tabasamu nene na picha za watu mashuhuri waliovaaa suti kali hivyo sitaliongelea sana suala hili hadi pale vitendo vitakapoanza kutendeka.

Suala moja walilolisahau kwenye G20 ni kuwahimiza watu wa Afrika kuwa wakaze uzi, waache uvivu na wapunguze utegemezi kwani jungu la wafadhili ipo siku litatakauka na watalala njaa kwa kuendekeza tabia ya kuombaomba. Siku ikifika kila mtu atajali watu wake kwanza na sio wananchi wa Mwanalugali! Tusiweke misaada ya wafadhili kama sehemu mojawapo ya miundo ya kujenga uchumi bora – hii dhana imepitwa na wakati.

Dk Kyaruzi akimkabidhi Balozi Mwanaidi Maajar nakala ...

Dk Kyaruzi akimkabidhi Balozi Mwanaidi Maajar nakala ...

KITOTO:

Turudi katika uandishi Tanzania. Mkuki na Nyota ni wachapishaji pekee wanaowakilishwa kidogo nje, wenye tovuti na wanaojitahidi. Je kitabu kinauzwa vizuri? Ulichapisha nakala ngapi? Je, wasomaji wengi wako nje au ndani? Unayo njia ya kuyajua hayo?Unaridhishwaje na hali ya uandishi na usomaji wa vitabu nchini.

Dk. Imani Kyaruzi:

Mkuki na Nyota wanao mpango wa kukiendeleza na kukisambaza kitabu hiki nchini kote. Kazi hii imeanza tayari na ninategemea mawasiliano hivi karibuni. Nakala zilizochapishwa ziko katika maelfu na ninaweza tu kuongelea wanunuzi wa bara la Ulaya. Wakati wa unzinduzi nilifanikiwa kusaini nakala nyingi sana na kitabu kilipokelewa vizuri na umati wa Watanzania waishio Uingereza. Baadhi ya nakala zilienda Ujerumani kwa wasomaji wa huko na marejesho yanaridhisha.

Nia ni kuwafikia wasomaji wa ndani na kazi hii itaanza baada ya majuma mawili. Ningependa kutoa mafunzo nyumbani wakati wa kukitangaza kitabu hiki.

Kuhusu uandishi na usomaji, inasikitisha sana kwani tumezoea kuona vitabu vya kina Michael Porter na kina Mr Smith na ninafikiri Watanzania tukianza kuandika italeta changamoto kwa waandishi walioko nyumbani ambao naamini wako wengi, tu. Kwa upande wa usomaji sina uhakika na hilo, ila tu ningependa kusisitiza kuwa vitabu vya mitaala hadi Chuo Kikuu viwakilishwe na vitabu vilivyoandikwa na wazalendo na vyenye kulenga katika hali halisi ya nchi. Hii ni muhimu kwani vitabu vyenye maudhui ya Kiulaya vinawatayarisha vijana wetu kutumikia nchi gani?

KITOTO:

Nini makusudi ya kuandika kitabu kuacha yale uliyoelezea mwanzoni (Utangulizi). Je, nini kilichokupa moyo au nia ya kuandika kitabu. Labda uliona hatusomi? Labda uliona wafanyabiashara Ulaya (kama bwana Richard Branson uliyemtaja) wanaandika vitabu?

Dk. Imani Kyaruzi:

Wakati wa ziara ya utafiti barani Afrika (Tanzania, Uganda, Ghana, Swaziland na Botswana) niligundua baadhi ya vitu vilivyokuwa vikkikwamisha biashara za wazalendo. Watu walikuwa wema sana na walichangia mawazo nami nilihaidi kutumia mapungufu yao, si kwa kuwaonyesha kuwa hawawezi bali kuwarudishia kitu fulani ambacho wanaweza kukitumia kuendeleza biashara zao. Je, ujumbe ningeufikishaje wakati walio wengi hawaongei lugha za kigeni? Nilionelea ni vyema kuanzia nyumbani, hivyo nikajikuta ninaandika kwa Kiswahili. Nia haikuwa kutengeneza faida bali kurudisha kitu kidogo katika jamii iliyonilea kwa mapenzi makubwa. Pia kuna wale watu wenye nia njema ya kujenga uchumi wetu lakini hawakubahatika kwenda vyuoni na wana nia ya kujiendeleza – hawa wanahitaji msaada wetu mkubwa kwani kama wote tungefanikiwa kwenda vyuoni basi baadhi ya biashara zisingekuwepo! Mama Ntilie aliyenipikia nikiwa Tambaza na Mzee Sefu wa Chips nao pia wasingenipatia lishe bora iliyonisukuma hadi leo naweza kuitwa Bwana Daktari. Lakini jambo muhimu hapa ni kwamba si lazima uende chuo kikuu kujifunza namna ya kutathmini faida katika biashara, unaweza kusoma kitabu hiki na kufuata mifano…Dk. Imani Kyaruzi

Dr. Imani Kyaruzi ni Profesa Msaidizi  katika Chuo Kikuu cha London Graduate School of Management…

KITOTO:

Sura ya Tatu muhimu sana; maana unaeleza “namna ya kupanga biashara.” Mantiki yako kwa maoni yangu mpitiaji ni kudokeza juu ya uholela na kutokuwa na nidhamu katika masuala yetu ya kikazi Bongo. Unafikiriaje kuhusu wafanyabiashara wetu. Je wana nidhamu, bidii na kujituma? Mbona Wakenya, Waganda na Wahindi wanatawala sana biashara zetu Tanzania?

Dk. Imani Kyaruzi:

Hii imenifurahisha sana! Kuna biashara za aina nyingi Bongo lakini zinazotawala ni zile za kina bwana Kauzeni – hajui tofauti ya rafiki na mteja, msambazaji na mzalishaji n.k Wote hawa huwaweka kundi moja na hata mtaji hajui alianzia wapi na kuishia wapi. Mifumo mingi ni kama ya genge – nyaya zikija unanunua tenga – zote mbivu, mbichi na zilizooza ; siku zikiharibika mtu anasema ni kudra ya Mungu, zikiuzwa zote anasema ridhiki imeingia. Watanzania wanajituma sana, tatizo ni nidhamu katika kazi na huduma kwa wateja. Waganda, Wakenya na Wahindi wanaweza sana kutawala biashara zetu kwani utamaduni wao unatofautisha biashara na sindimba. Wakiwa katika biashara uhusiano wao hubadilika na hufuata kanuni za biashara na wakati wa sindimba kanuni zinazotumika ni zile za midundo. Lakini tumeanza kubadilika – tunaweza kujifunza kutoka kwa hawa wenzetu; ila tusijifunze kila kitu kwani tabia zingine za wageni si za kuiga.

KITOTO:

Je unaamini ubepari utaleta maendeleo Tanzania? Yaani ukilinganisha enzi za Ujamaa (1967-1986) na Mwalimu Nyerere?

Dk. Imani Kyaruzi:

Duh! Tanzania sio nchi ya Kijamaa na wala sio nchi ya Kibepari bali iko tu katika hatua za kusahau nasaha za ujamaa na kuuelekea ubeparini – tumeacha tu kuvaa kaunda suti lo! Kutokuwa na msimamo kamili ndo’ kunaleta utata juu ya faida na hasara za mifumo hii katika kuleta maendeleo. Kuna vitu viwili hapa – siasa zinajenga uchumi au uchumi unajenga siasa. Bwana mwandishi enzi za Nyerere siasa za ujamaa zililenga katika kujenga uchumi ulio bora na wenye uwiano. Sasa baada ya kifo cha ujamaa hadi leo hii uchumi ndio unaamua siasa gani ufuate! Sasa tukirudi katika swali lako jibu ni hapana na ndio! Ubepari utaweza kuleta maendeleo kwa watu wachache tu wanaojua kucheza katika anga za ubepari, walio wengi hawajui na hawatajua nini kinaendelea na wanaweza kuuzwa kwa bei ya jumla. Ubepari nia yake ni kulimbikiza mali na si rahisi kujenga uwiano – hapa ni rahisi kujenga jamii mbili za wazalishaji na walaji na mara nyingi masikini ndio wanakuwa wazalishaji. Kwa upande wa pili, ubepari unaweza kuleta maendeleo kwa kuendeleza ushindani. Kama nilivyoeleza katika kitabu, ushindani ni wa muhimu sana katika kujenga jamii yenye ari ya kujituma na kuzalisha bidhaa na huduma bora. Tatizo labda la huu ushindani ni kuwa mara nyingi unakuta washindanaji wana nguvu zisizowiana – kwa mfano Steers na Mama Hassan wa Sinza wakiamua kutengeneza vitumbua Mama Hassan atashindwa kwani hajaendelezwa au kuwezeshwa japo kufikia nusu ya kiwango cha mshindani wake. Maana yangu ni kwamba kabla hujaruhusu ushindani nyumbani kwako lazima uhakikishe wapiganaji wako umewalisha vizuri la sivyo nyumba yako inaweza kutawaliwa na wageni.

Sasa nini kifanyike! Kwa mtazamo wangu ubepari si mbadala halisi wa ujamaa. Baada ya mfumo wa ujamaa kufumuka tulitakiwa kusuka mfumo wetu wa ubepari ambao hauna matobo mengi kama tulionao sasa. Huu mfumo wetu wa sasa wa Pseudo-capitalism au wengine wanaita a transition to a market-led economy misingi yake ni ile ya kula kuku, mayai, manyoya na hata mbolea kistaarabu huku wananchi wakizidi kuumia. Maendeleo ya ubepari utayaona Oysterbay na Masaki lakini huko Mwanalugali sahau kabisa – maendeleo yatakuwa ni barabara za kupitisha mchanga wa kujenga nyumba za mapumziko ya wikiendi. Tutataendelea kupita huku watoto wadogo wenye kamasi vifua wazi wakiendelea kupungia magari yetu makubwa kama nyumba. Hatutasikia kelele zao kwani vioo vitakuwa vimefungwa ili hewa iliyochujwa isichanganyike…

WASILIANA NA MWANDISHI KUPATA NAKALA AU HABARI ZAIDI :

Simu : +44 -7977807295

Barua pepe: boraimani@yahoo.com

MPE MANENO YAKE…

 

fab-moses-pic by f macha

Si wanamuziki wengi wanaoishi ughaibuni toka Bongo.  Miaka mingi hata hivyo  amekuwepo mtunzi na mwimbaji, Fab Moses ,  CD na shoo yake inayoitwa NENGUA.

Mtazame katika tovuti  ya My Space:

http://vids.myspace.com/index.cfm?fuseaction=vids.individual&VideoID=42998197

Mbali na nyimbo zake mathalani: “Ngunguri Ngangari” na “Nyerere” , Fab Moses huonekana katika majukwaa kadhaa ya London akitungua nyimbo mbalimbali za Kiswahili na bendi mashuhuri ya Afrika Jambo.  Bendi hii inasimamiwa na magwiji Kawele “Finger Printer”Mutimanwa, mpiga gitaa mashuhuri wa Kikongo, Uingereza na Ramadhani Athumani Mtunguja (”Rama Sax”) mpiga saxafoni mzawa wa Tanga aliyekuwa zamani na Simba wa Nyika na Les Wanyika na kushikiri katika kibao maarufu Sina Makosa kilichotolewa Nairobi mwaka, 1978. Afrika  Jambo hutumbuiza klabu kadhaa mashariki ya London zikiwemo (East Side Bar, Ilford) Kila Jumapili na Railway Tavern klabu ya Waganda, Forest Gate.

Waliomsikia Fab Moses huvutiwa na uzuri wa sauti yake inayokumbusha vibao mbalimbali vya nyumbani kama nyimbo za Shabani Marijani (Georgina), Simba wa Nyika, Mlimani Park, nk. Moja ya Sifa anazopewa Fab Moses ni sauti inayolandana sana na ya mwanasokomoko, hayati Marijani.

Mwanamuziki Fab Moses ni vile vile mwanasarakasi wa siku nyingi aliyeshafanya kazi na vikundi kadhaa nyumbani ikiwepo Muungano (cha Mzee Nobert Chenga) na Black Eagles. Kwa takribani miaka minane sasa anaongoza kikundi chake cha sarakasi na michezo jukwaani kinachoitwa Highflyers. Walioshamshuhudia (nikiwemo) wanakubali Fab Moses ni  mwalimu na kocha mzuri sana wa Sarakasi. Chini ya utaalamu wake mtu yeyote (watoto kwa wazima) anaweza kufundishwa kujinyonga nyonga na kuwa mwanasarakasi. Hilo latokana na uvumulivu na ufundi wake, Mtanzania huyu mwenye vipaji vingi…

fab-moses-singing

Habari zaidi za NENGUA, kikundi cha Sarakasi (Highflyers) au Afrika Jambo; mpigie Fab Moses -+44-7950-604530

Barua pepe: fabrahs@yahoo.co.uk

Picha na Freddy Macha

Mwezi Novemba mwaka huu ulikuwa wa kheri na baraka kwa jina la Tanzania nchi za nje. Badala ya mabaya kuongelewa (mathalani mauaji ya Ma-albino) au mazuri (Amani ukilinganisha na Waafrika wenzetu) kutoongelewa; tukaWIKA KIJOGOO. Kidesturi, kihistoria na kifani, Tanzania haitangazwi ughaibuni; kwa walioshasafiri safiri mnafahamu (na kujionea) vipi bado wanatuita Tasmania au Kenya; hatujulikani. 

Kwa siku nne lakini ; kama picha zinavyoonyeshwa chini, kila aliyekuwepo aliona fahari kuwa Mbongo…nimezunguka nchi nyingi na kuona mengi; lakini sijapata kushuhudia kitu kama hiki…

Ngoma ni moja ya misingi mikuu ya asilia yetu; na jamaa wa Sisi Tambala wakiongozwa na Kibiriti Nanjuja walionyesha taswira nzuri kuiweka mbele; huku wakisindikizwa na magitaa. Kwa maoni yangu, sura hii ndiyo inapaswa kuitwa muziki wa kizazi kipya. Aghalabu muziki huu unaofanya mchuzi mseto wa juzi, jana na leo ndiyo utakaotuweka katika ramani ya Usanii wa Kuheshimika duniani. Wenzetu wa Afrika Magharibi (na Kusini) washang'amua hayo zamaaaaaani! Ndiyo maana wako kilometa nyingi mbele yetu...

Ngoma ni moja ya misingi mikuu ya asilia yetu; na jamaa wa Sisi Tambala wakiongozwa na Kibiriti Nanjuja (aliyebeba ngoma) walionyesha taswira nzuri kuiweka mbele; huku wakisindikizwa na magitaa. Kwa maoni yangu, Uso huu ndiyo unapaswa kuitwa muziki wa Kizazi Kipya. Aghalabu sanaa hii unayopika mchuzi (na kuku) wa juzi, jana na leo ndiyo utakaotuweka katika ramani ya Usanii wa Kuheshimika duniani. Wenzetu wa Afrika Magharibi (na Kusini) washang'amua hayo zamani SANA.

Wanamuziki wa Sisi Tambala wakishabikiwa (kuzidi kiasi) na jamaa huyo aliyeshindwa kujizuia toka Ulaya Mashariki...

Wanamuziki wa Sisi Tambala wakishabikiwa (kuzidi kiasi) na jamaa huyo aliyeshindwa kujizuia toka Ulaya Mashariki...Aliye kifua wazi ni mpiga Kit Drums (ngoma za vijiti) Omari Ali Cosmas. Mbali na kipaji chake huyu bwana huwa haachi kutabasamu jukwaani. Labda ndio kisa cha kushabikiwa vile. Sura Ya Bongo ni Urafiki. Uswahiba.

Gloria Mutahanamilwa wa gazeti la Watanzania London (TZUKNET) alikuwemo bila shaka...

Gloria Mutahanamilwa wa gazeti la Watanzania London (TZUKNET) alikuwemo bila shaka yeyote...

Dumange Thomas; mcheza dansa wa Sisi Tambala akipumzika huku akitengeneza nywele ...yeye na mwenzake Yuster walikuwa maua muhimu sana kufanikisha maonyesho haya ya siku nne...
Dumange Thomas; mcheza dansa wa Sisi Tambala akipumzika (huku akitengeza nywele) …yeye na mwenzake Yuster walikuwa maua muhimu sana kufanikisha maonyesho haya ya siku nne…
Amant Macha wa Shirika la Utalii Tanzania akisambaza matangazo na vijarida vya kutangaza nchi. Maonyesho haya ya kimataifa ni muhimu sana kibiashara kwetu...

Amant Macha wa Shirika la Utalii Tanzania akisambaza matangazo na vijarida kwa maelfu ya waliohudhuria Excel kutangaza nchi. Maonyesho haya ya kimataifa ni muhimu sana kibiashara...

Ignus Kapyunka wa Sisi Tambala; akicharaza besi...vituuuuuu!
Ignus Kapyunka wa Sisi Tambala; akicharaza besi…vituuuuuu!
Colette Shannon na mumewe Kevin; jamaa hawa wa Cornerstone walichangia sana kufana kwa jina la Tanzania katika maonyesho haya. Collette anasema Tanzania ni nchi nzuri lakini haijajitangaza ipasavyo.
Colette Shannon (mzawa wa Mauritius) na mumewe Kevin (mzawa wa Zimbabwe); jamaa hawa wa Cornerstone walichangia sana kufana kwa jina la Tanzania katika maonyesho haya. Collette anasema Tanzania ni nchi nzuri lakini haijajitangaza ipasavyo.
James Nanjuja (mwanae Kibiriti Nanjuja, wa Sisi Tambala) akiyatandika Marimba; muziki wa Kijadi uliochanganywa na vyombo vya kisasa ndiyo utakaotupeleka mbali Watanzania kimuziki.
James Nanjuja (mwanae Kibiriti Nanjuja, wa Sisi Tambala) akiyatandika Marimba; Ala za Kijadi zinazochanganywa na vyombo vya kisasa ndiyo zitakazotupeleka mbali Watanzania, kimuziki.
Aron Richard, mpiga gitaa wa Sisi Tambala akiwa kazini...
Aron Richard, mpiga gitaa wa Sisi Tambala akiwa kazini…
Tangazo la Tanzania (Nchi ya Serengeti, Kilimanjaro na Zanzibar) ambalo limekuwa likivimba na kuwasha kibiriti katika sehemu mbalimbali muhimu mjini London miezi ya karibuni...zamani ilikuwa Kenya ndiyo inaonekana tu. Tunaanza kuamka kidogo kidogo...

Tangazo la Tanzania (Nchi ya Serengeti, Kilimanjaro na Zanzibar) ambalo limekuwa likivimba na kuwasha kibiriti katika sehemu mbalimbali muhimu mjini London miezi ya karibuni...zamani ilikuwa Kenya ndiyo inaonekana tu. Tunaanza kuamka kidogo kidogo...

Zubeda (Uganda) na Mutsa (Zimbabwe) wachezaji shoo wa bendi ya Kitoto waliostarehesha nami siku hiyo...hatukujivunga.
Zubeda (Uganda) na Mutsa (Zimbabwe) wachezaji shoo wa bendi ya Kitoto waliostarehesha nami siku hiyo…hatukujivunga.
Viazi vya kukaanga (chips) chakula kikuu cha Waingereza; Chapati (chakula cha Wahindi), Nyama choma, bia za Serengeti na Dodoma Wine ni moja ya makulaji yaliyotolewa bure kwa wageni na Wabongo waliohudhuria tafrija hii mufti...
Sambusa na Chapati (vyakula vya Wahindi ambavyo vimeshakuwa utamaduni wetu), Nyama choma, bia za Serengeti na mvinyo wa Dodoma Wine ni moja ya makulaji yaliyotolewa “bure” kwa wageni na Wabongo waliohudhuria tafrija hii mufti…
Moja ya mambo yaliyovutia sana kadamnasi ni raia huyu Mzungu toka Ukraine aliyeshindwa kujizuia akawa anataka kuzidunda ngoma za bendi ya Sisi Tambala mwisho mwisho wa shughuli. Ilibidi atolewe mkuku na wana usalama. Mapenzi ni kikohozi hayapendi kufichama. Ama kweli Bongo ilitia fora.
Moja ya mambo yaliyovutia sana kadamnasi ni raia huyu Mzungu toka Ukraine( Andria) aliyeshindwa kujizuia akawa anazidunda ngoma za bendi ya Sisi Tambala mwisho mwisho mwa shughuli. Ilibidi atolewe mkuku na wana usalama. Mapenzi ni kikohozi hayapendi kufichama. Ama kweli Bongo ilitia fora.
Geoffrey Meena wa Shirika la Utalii na Yuster Kari wa Sisi Tambala
Geoffrey Meena wa Shirika la Utalii na Yuster Kari wa Sisi Tambala
Mdau wa Kitoto nikiwa na Kiongozi wa Sisi Tambala, Kibiriti Nanjuja
Mdau wa Kitoto nikiwa na Kibiriti.
Collette Shannon, Mkurugenzi wa Shirika la Cornerstone London na Katibu Mkuu katika Wizara ya Utalii na Mali Asili, Blandina Nyoni, waliokuwa kiini cha mafanikio haya.
Collette Shannon, Mkurugenzi wa Shirika la Cornerstone London na Katibu Mkuu katika Wizara ya Utalii na Mali Asili, Blandina Nyoni, waliokuwa kiini cha mafanikio haya.
Yuster na Dumange wakionyesha fahari na uzuri wao kufaidisha taswira ya Bongo nje...
Wacheza shoo wa bendi ya Sisi Tambala: Yuster na Dumange wakionyesha fahari na uzuri wao kufaidisha taswira ya Bongo nje…
Ayoub Mzee wa Ben TV (aliyekuja kutangaza kihabari); Yusufu Kashangwa (Mkutugenzi wa Tanzania Trade Centre) aliyekuwa mmoja wa wahusika si tu mwaka huu bali miaka mingi iliyopita kuitangaza nchi nje; na Juma Makabila, mtaalamu wa masoko.
Wataalamu wetu London waliohudhuria : Ayoub Mzee wa Ben TV (aliyekuja kutangaza kihabari); Yusufu Kashangwa (Mkurugenzi wa Tanzania Trade Centre) aliyekuwa mmoja wa wahusika si tu mwaka huu bali miaka mingi iliyopita kuitangaza Bongo nje; na Juma Makabila, mtaalamu wa masoko.
kulia kwake Kiongozi Kibiriti Nanjuja
Andria toka Ukraine aliyeshabikia wana Sisi Tambala.

Older Posts »